Karibu Wilaya ya Bukombe

Wednesday, November 8, 2017

Bukombe Yaendelea Kung'ara


Bukombe imekuwa katika jitihada za kuendelea kuboresha utoaji huduma kwa jamii katika sekta mbalimbali ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kutekeleza mipango ya bajeti.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa hivi karibuni na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Halmashauri ya wilaya ya Bukombe imekuwa ya Pili kwa Mkoa wa Geita katika Utoaji huduma bora kwa wananchi kwa kuzingatia Sera,Kanuni, na viwango vilivyowekwa kwa kila sekta ya huduma za jamii hususani katika sekta  za Afya,Maji,Elimu,Barabara na Usimamizi wa Fedha.

Takwimu hizi zimejikita katika matumizi sahihi ya fedha kwa ujumla kwa kutumia taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG) ya Mwaka 2015/2016 pamoja na taarifa ya kamati ya Hesabu za serikali za Mitaa.

Katika mchanganuo huo Halmashauri ya wilaya ya Bukombe imeshika nafasi ya pili katika  Mkoa wa Geita kwa jumla ya alama 60.83 ikitofautiana kwa alama 11.94 tu na Halmashauri iliyoongoza Kitaifa yenye jumla ya alama 72.73.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Bukombe anapenda kuwashukuru wananchi wote ambao ndiyo wadau wakubwa wa maendeleo wilayani hapa  katika kufanikisha utekelezaji makini wa shughuli zote za kila siku.
Aidha changamoto hazikosekani hivyo tunaahidi kuboresha huduma bora na za kisasa kwa kushirikiana na wananchi ili kuhakikisha tunazipunguza kama si kumaliza kabisa changamoto zinazojitokeza kwa sekta zote kwa maelekezo ya serikali ya awamu ya tano.

                 TUSHIRIKIANE WANA BUKOMBE 2017.

IMETOLEWA NA;
KITENGO CHA TEKNOLOJIA, HABARI NA MAWASILIANO.
BUKOMBE

8/11/2017

Pongezi Miaka Miwili kwa Uongozi wa Awamu ya Tano.

Bukombe yaungana na wananchi wote Tanzania kutoa  Pongezi kwa Uongozi wa awamu ya Tano wa Mhe.Rais John Joseph Pombe Magufuli katika kipindi cha Miaka Miwili mabadiliko makubwa yamefanyika ambayo yanapeperusha vizuri bendera ya Tanzania. Mungu endelea kubariki Viongozi wote,wananchi kwa ujumla wake ili gurudumu la maendeleo lisonge mbele.

Friday, October 27, 2017

Asali yaing'arisha Bukombe Maadhimisho ya Chakula Duniani Mkoani Geita.


Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Taifa (FAO) na Shirika la Mpango wa Chakul duniani (WFP) yavutiwa sana na zao la Nyuki (Asali) pamoja na zao la Muhogo kutoka wilaya ya Bukombe katika maonyesho ya siku ya Chakula yaliyofanyika Mkoani Geita.
Na hivyo kuamua kutembelea wilaya ya Bukombe kujionea Uzalishaji wa mazao hayo katika uhalisia wake ili kutimiza dhana ya Uanzishwaji wa Viwanda kwa kukaribisha wawekezaji.  
Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Mhe.Josephat Maganga akiongea na wageni waliofika Ofisini kwake kutokea Shirika la  Mpango wa Chakula Duniani (WFP) na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Taifa (FAO)pamoja na The International Institute of Tropical Agriculture (IITA).

Mwakilishi Mkazi kutoka Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Bi. Neema Sitta katika Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Bukombe.

Mwakilishi Mkazi kutoka Shirika la Chakula na Kilimo Umoja wa Taifa (FAO) Bwana. Fred Kaferelo katika Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Bukombe.

Dr Fred Baijyuka kutoka kutoka The International Institute of Tropical Agriculture (IITA)  akijitambulisha alipofika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Bukombe kwa lengo la kuona Soko la Zao la Muhogo wilayani hapa.


Katika ziara hii ya wageni kutoka Mashirika ya Chakula walifika na kutaka kujionea uhalisia wa uzalishaji wa zao la Nyuki yani Asali na Nta.
Kwa mwaka jana vikundi mbalimbali vya uzalishaji Asali wilayani hapa viliweza kuzalisha Tani 300. Mwaka huu  kuanzia mwezi wa 7 mpaka sasa tani 237 zimesafirishwa nje ya nchi na Tani 76 zimesafirishwa ndani ya Nchi. Pamoja na zoa linguine la Nyuki Yani Nta Tani 22 imesafirishwa  ndani ya nchi.

Hizi ni Asali ambazo zipo kwenye Vifungashio tayari kwaajili ya kuuzwa madukani,sokoni. Asali inayoonekana Nyesui sana ni Nyuki wadogo na sali inayoonekana sio Nyeusi ni Nyuki wakubwa.
Afisa Nyuki wilaya ya Bi.Dafroza Shayo akifafanua uzalishaji  wa zao la Nyuki (Asali) kwa wageni kutoka mashirika mbalimbali yanayohusiana na Chakula na Kilimo wilayani Bukombe.
Mzalishaji wa Asali kutoka kijiji cha Msonga kata ya Runzewe Mashariki Bwn. Obadiah akizungumza namna anavyozalisha zao hili la Nyuki.
Baadhi ya Madumu yaliyojaa Asali.
Madumu na Ndoo lita 20 zilizojaa Asali kwaajili ya kuanza kuchunjwa.

Hapa ndipo Asali inapochunjiwa ili kuweza kwenda hatua nyingne ya mwisho ya kuchuja na tayari kuwekwa kwa vifu,ngashio.


Vipaumbele vya Halmashuri ya wilaya ya Bukombe ni kuendelea kuibua miradi ya maendeleo kwaajili ya maendeleo ya wilaya. Mradi wa Soko la Mihogo ni kwa maendeleo ya wana Bukombe wanaolima sana zao la Muhogo ambalo limekuwa likihitajika sana katika nchi za jirani Uganda,Rwanda,Burundi na Demokrasia ya Kongo.
Afisa Kilimo Bwn.Joseph Machibya akielezea mradi wa Soko la Mihogo lililopo kata ya Namonge wilayani hapa kwa wageni waliofika kulitembelea.

Hili ndilo Soko la Kimataifa la zao la Muhogo lilipo kata ya Namonge wilayani Bukombe ambalo lilipata nafasi ya kutembelewa na wageni kutoka Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Taifa (FAO) ,Shirika la Mpango wa Chakula Duniani(WFP) na The International Institute of Tropical Agriculture (IITA) ili kuona fursa za Uwekezaji katika uanzishaji wa Viwanda wilayani hapa. 
Sehemu ya Kuweka Macao kwa wafanyabiashara wa Soko hili.
Meza za  kuwekea zilizojengwa katika Soko hili.
Hili ndilo Jengo la kuwekea mazao kwaajili ya kuuza nan je halo ni kichujio cha zao la Muhogo Baada ya Kuoshwa ili maji yakauke.

                               Maghala ya Kuhifadhia Mazao katika Soko la Mihogo .

Monday, October 23, 2017

Semina ya Kuongeza Uelewa juu ya Ualbino na Kupinga mauaji ya watu wenye Ualbino yafanyika wilayani Bukombe.

Mwenyekiti wa Chama cha watu wenye UALBINO Tanzania  (TAS- BUKOMBE) Bi.Ida Saka amekemea vikali mauaji yanayoendelea kwa watu wenye ualbino Tanzania.
 Amesema hayo kwenye warsha ya Mradi Jumuishi wa watu wenye ualbino iliyofanyika wilayani Bukombe ikishirikisha wadau mbalimbali yakiwemo madhehebu ya dini,waganga wa jadi,watumishi wa serikali huku Mgeni Rasmi akiwa Mkuu wa wilaya ya Bukombe aliyewakilishwa na Ndugu Ally Mketo Afisa Tawala wa Wilaya.


Mwenyekiti wa Chama cha  watu wenye Ualbino Bukombe Bi.Ida Saka.
Mgeni Rasmi aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Bukombe ambaye ni Afisa Tawala Ndugu Ally Mketo.
 Amesema “Watu wenye Ualbino wana haki sawa kama wanadamu wengine na wana uwezo wa kusoma,kufanya kazi,kuishi inashangaza sana kuona vitendo vya kikatili vinafanywa na watu ambao mimi nasema hawana Hofu ya Mungu, Mimi kwetu Babu yangu ni Albino lakini mbona mimi mjukuu wake si Albino,Ndugu zangu elimu tutakayo pata hapa tuifikishe na kwa wengine ili ukatili ukome kbsa.
Mratibu wa Mradi Jumuishi wa watt wenye Ualbino wilaya ya Bukombe Ndugu Emmanuel Simon.
Mwezeshaji wa Mradi Jumuishi wa watu wenye Ualbino ambaye pia ni Mwalimu wa Somo la Biology katika Shule ya Sekondari Runzewe Ndugu  Simon Mashauri   akitoa maswali kwa vikundi baada ya kufundisha nini Maana ya  Neno “Albino”, mtu anakuaje Albino,Haki za watu wenye Ualbino,Sheria ya Makosa ya Jinai na Sheria ya watu wenye Ulemavu ya  No.9 ya mwaka 2010.
Mtoto Hamad nae alikuja kwenye semina na Mama yake Bi.Halima .


Mganga wa Jadi Bi.Sada akiwa akisema Jambo wakati wa semina  ya mradi jumuishi  wa watu wenye Ualbino.

Afisa Mipango wa Wilaya Bi.Sarah Yohana na Afisa Maendeleo ya Jamii Bi.Prisca Lyimo wakisikiliza semina ya Mradi Jumuishi wa watu wenye Ualbino.

Viongozi wa Kidini Kutoka Madhehebu mbalimbali nao wakisikiliza Semina Jumuishi katika Ukumbi wa Halmashauri.
Diwani wa Kata ya Katente Mhe.Bahati Kayagila akichangia mada katika semina ya Mradi Jumuishi wa watu wenye Ualbino amesema “Watu wenye Ualbino wana haki zote sawa na watu wasiokuwa na ualbino ni muda sasa wa kuendelea kupambana na watu wakatili  kila mmoja atoke humu na kusambaza elimu hii na tukawe wa fuatiliaji wa matukio haya ya kikatili” amesisitiza
Kazi za Vikundi baada ya Kupewa maswali na muwezeshaji.
Bi. Eliwaje Wa Dawati  la Jinsia wilaya ya Bukombe.


Kazi ya Vikundi ikiendelea ambapo vikundi vine kwa awamu mbili zilijibu maswali ya mwezeshaji na kuwasilisha.

Tuesday, July 11, 2017

Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Benjamin Mkapa akimkabidhi Hati za Umiliki wa nyumba 10 za Watumishi wa Afya wilayani Bukombe.

Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Mhe.Benjamin Mkapa amekabidhi Hati za Umiliki wa nyumba 10 za Watumishi wa Afya wilayani Bukombe zilizojengwa na Taasisi ya Mkapa (Mkapa Foundation) katika vijiji vya Uyovu,Bulega,Bugelenga,Msasani na Miyenze.
Hafla hiyo ya makabidhiano imefanyika katika uwanja wa Mazaina Chato mkoani Geita ikiwalisha wilaya zote za Mikoa ya Geita, Simiyu na Kagera  zilizopata ufadhili wa ujenzi wa nyumba za watumishi wa afya. 
Wakati wa kukabidhi Nyumba 50 Mhe.Mkapa ametoa pongezi kwa jitihada za uboreshaji wa huduma za afya zinazofanywa na serikali ya awamu ya tano ya Mhe.Rais John Joseph Pombe Magufuli.Taasisisi ya Mkapa  itaendelea kushirikiana na serikali katika kuimarisha utoaji wa huduma za Afya kwa kushirikiana na Mfuko wa Dunia unaopambana na ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukimwi, Ujenzi wa Nyumba hizo ni chachu ya uwajibikaji,uadilifu kwa watoa huduma ambao ni watumishi wa Afya, "Madaktari hakikisheni mnafanya kazi kwa kuafata taratibu za kazi na kuzingatia haki za binadamu" amesema Mhe.Mkapa.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Mkapa Dkt.Ellen Senkoro wakati akitoa Taarifa ya taasisi ameeleza kuwa  taasisi hiyo ni asasi isiyo ya kiserikali ambayo imekuwa ikishirikiana na serikali za Mitaa na imeweza kutoa ajira takribani 1,100 kupitia Sekretarieti ya ajira,ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wasiojiweza 949, ujenzi wa Nyumba 50 za watumishi wa Afya katika Mikoa ya Geita ambapo nyumba 20 zimejengwa, 10 zimejengwa Kagera na  20 zimejengwa Simiyu na mikoa mingine ambio talari wamekabidhiwa ni katika jitihada za kuhakikisha watoa huduma wa Afya wanakaa katika Nyumba zenye mazingira mazuri ili kutoa huduma bora na kwa wakati. Bi.Senkoro ameongeza katika juhudi za kupunguza vifo vya wakina Mama wajawazito ambapo vyumba vya upasuaji (theatre) 11 katika vituo vya Afya vimejengwa.
Dkt.Senkoro amefafanua kuwa taasisi hii iliingia Mkataba wa kujenga Nyumba 480 ambapo nyumba 430 zimekamilika na nyumba 30 zinatarajiwa kukamilika mwezi Agost, kupitia mfuko huu wa Dunia(Global Fund) unaopambana na ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukimwi,  Mikoa 17 na Halmashauri 51 zimeweza kufikiwa na vituo  vya Afya 268 vimejengwa. Katika Halmashauri ya Chato,Bukombe,Maswa, na Biharamulo ujenzi umegharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 2.5 wastani kila nyumba 1 ni Shilingi Milioni 35, ambapo Nyumba 22 zinatumia umeme wa kawaida na nyumba 28 zinatumia umeme wa jua. Mtendaji Mkuu wa Taasisi hiyo ametoa shukrani kwa ushirikiano mzuri uliopo kati ya Wizara ya Afya,Jinsia na Maendeleo,Mfuko wa Dunia pamoja na Serikali za Mitaa.
Mfuko wa Dunia unashirikiana na serial ya Tanzania tangu mwaka 2003 na mwaka  huu 2017 mfuko umeingia mikataba 16 yenye jumla ya thamani ya shilingi Trillioni 3.8 kwaajili ya kupambana na Kifua Kikuu na Ukimwi, vigezo vya utendaji vimezingatiwa na Tanzania ni moja kati ya nchi zinazotekeleza vyema malengo ya Mfuko wa Dunia ambayo ni kuboresha huduma za afya, mwishoni mwa mwaka 2016 takribani watu laki 7 wamepatiwa dawa za kupunguza makali ya Ukimwi,na katika kuendelea kupunguza maambukizi ya ukimwi condom milioni 38 zimesambazwa kupitia mfuko wa dunia. Aidha mfuko wa dunia kwa kushirikiana na serikali imejenga maghala ya kuhifadhia dawa, ufadhili wa masomo na ujenzi wa nyumba 480 kushirikiana na Mkapa Foundation pamoja na Serikali ya Tanzania. "Mfuko wa dunia unaridhishwa na Serikali ya Tanzania kwa kutekeleza yote yaliyokusudiwa na Mfuko huo " amesema Mwakilishi wa Mfuko wa Dunia (Global Fund) Bi. Matha Setembo.

Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Benjamin Mkapa akizungumza na wananchi wa Mikoa ya Geita, Simiyu na Kagera katika uwanja wa Mazaina Chato mkoani Geita kabla ya kukabidhi Hati za umiliki wa nyumba 50 za watumishi wa sekta ya Afya zilizojengwa na Taasisi ya (Mkapa Foundation) katika mikoa hiyo mitatu. 
Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Benjamin Mkapa akimkabidhi Hati za Umiliki wa nyumba 50 za Watumishi wa Afya kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu katika uwanja wa michezo wa Mazaina Chato mkoani Geita.

Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Benjamin Mkapa akabidhi Hati za Umiliki wa nyumba 10 za Watumishi wa Afya Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Bukombe Mhe.Safari Nicas Mayala.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimshukuru Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Benjamin Mkapa mara baada ya kukabidhi nyumba hizo 50 zitakazotumika katika Sekta ya Afya katika mikoa ya Kagera, Simiyu na Geita.
Wananchi wakifuatilia Hafla ya Makabidhiano ya Nyumba 50 kwa Mikoa ya Geita,Simiyu na Kagera yaliyofanyika Wilaya ya Chato Mkoa wa Geita.
Kikundi cha ngoma za asili cha Chato kikitumbuiza katika uwanja wa Mazaina Chato mkoani Geita.

Monday, April 3, 2017

Kiasi cha shilingi milioni 11.9 za wanakijiji zajenga vyumba viwili vya madarasa katika shule ya msingi Ihurike wilayani Bukombe




Mkuu wa Wilaya ya Bukombe  Mhe.Josephat Maganga afungua rasmi vyumba viwili vya madarasa   shule ya msingi Ihurike .

Mhe. Maganga amesema amefurahishwa sana na tafsiri nzuri kuhusu Elimu bure ambapo wananchi wanashiriki  kuchangia kwa hali na mali ili kuongeza na kuboresha miundombinu ya elimu.
"Hili ni suala la kujivunia sana, kuona juhudi za serikali zikipata ushirikiano kutoka kwa wananchi, naombeni tusiishie hapa twende hivi hivi na katika miradi mingine ya maendeleo" amesema Maganga.





Aidha pongezi za dhati ziwaendee viongozi wa vijiji, Diwani wa kata ya Ushirombo Mhe.Lameck Warangi na Mbunge wa Bukombe Mhe.Doto Biteko kwakuwa viongozi bora wenye ushawishi mzuri wa kuleta Maendeleo katika Elimu wilayani kwetu, kwa pamoja sasa tuendelee kuwa watu swenye kujivunia maendeleo yetu na kuendelea kushirikiana kuboresha miundombinu yetu ya Elimu na Afya." ameongeza Mhe. Maganga.




Diwani wa kata ya Ushirombo Mhe.Lameck Warangi amedhirisha furaha yake kwa wana Ihurike kukamilisha ujenzi huu wenye thamani ya shilingi milioni 22.9 ndani ya siku 60 ikiwa nguvu za wananchi shilingi milioni 11.9 na Serikali kuu ni shilingi milioni 11.



"Wananchi wangu tuendelee kupambana ili kuleta maendeleo ya kielimu na kiuchumi katika vijiji vyetu nasema haya sababu mwenyeviti kutoka vijiji vingine kwenye kata yangu mpo hapa na mmejionea ujenzi huu wa miundombinu ya elimu niiteni nitakuja , maendeleo ya vijiji vyetu huletwa na sisi wenyewe tuchape kazi na pia tuendelee kumshirikisha Mbunge wetu wa Bukombe Mhe.Doto Biteko katika mikakati yetu ya maendeleo,Mbunge wetu anapenda maendeleo atatusaidia na kutuongoza vyema tumpe shukrani zetu za dhati katika kukamilisha maendeleo haya" amesema Mhe. Warangi



Shule ya Msingi Ihurike ina jumla ya wanafunzi 427, wavulana wakiwa 201 na wasichana 226 na walimu 9, pia ina choo kimoja chenye matundu 4,upungufu ukiwa ni matundu 8 kwa wanafunzi wa kike na matundu 6 kwa wanafunzi wa kiume, huku walimu wakiwa hawana choo kabisa na ni shule inayopakana na hifadhi ya msitu wa Kigosi Moyowosi.


Sunday, November 20, 2016

Mvua Kali iliyoambatana na Upepo mkali yaleta maafa wilayani Bukombe kata ya Namonge.


Kata ya Namonge wilayani hapa imekumbwa na maafa baada ya mvua kubwa ya muda mfupi iliyoambatana na upepo mkali ilionyesha majira ya saa 10 jioni siku ya jumatano ya tarehe 16/11/2016 . Mvua hiyo imeezua na kubomoa nyumba 132 ambapo kati ya hizo nyumba 47 zimeharibiwa kabisa, mvua hiyo pia imejeruhi watoto 5 waliyokuwa katika maeneo tofauti ambapo majeruhi wanne wanaendelea na matibabu katika kituo cha Afya cha Uyovu.

Mvua hiyo pia imeharibu miundombinu mbalimbali ya taasisi za serikali ikiwemo Vyumba vitatu vya madarasa, choo cha Walimu, nyumba ya Mwalimu ilipata mtikisiko na kunyanyua paa ambalo tayari limerudishiwa katika Shule ya Msingi Namonge. Aidha Miundombinu  mingine ya taasisi za kidini imeharibiwa na mvua hiyo makanisa  ya TAG, ANGLIKANA na PENTEKOSTE.



Vitongoji vilivyoathirika na mvua hiyo ni Namonge A nyumba 66, Namonge B nyumba 36, Kazilambwa nyumba 15 na Mwambakikulu nyumba 15, ghala la kuhifadhia Tumbaku la chama cha Msingi Namonge limebomoka na ghala lingine la mfanyabiashara anayejulikana kwa jina la Masanganya nalo limeezuliwa.









Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bukombe pamoja na Kamati ya Maafa  wamefika eneo la tukio kujionea hali halisi ya maafa ambapo Ndugu Paul Cheyo  kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Bukombe ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya maafa ya wilaya amewapa pole  watumishi , mabalozi na wananchi wote ambao wameathirika na madhara yaliyosababishwa na mvua hiyo na amewashukuru wananchi kwa kuwa na moyo wa kusaidiana wakati wa matatizo.

Kamari ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bukombe yatembelea Majeruhi kujua hali zao baada ya kupata madhara hayo yaliyoletwa na mvua kali iliyoambatana na upepo mkali.

 Ndugu Paul Cheyo Katibu Tawala wa Wilaya akimuangalia kwa umakini mtoto Timotheo Sospeter mwenye umri wa miaka 13 mwanafunzi wa shule ya Msingi Namonge darasa la 4 ambaye alipata majeraha chini ya kidevu,monomi na kichwani hali yake inaendelea vizuri.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Bukombe Ndugu Dionis Myinga akipata maelezo ya hali ya mtoto Daudi Charles mwenye umri wa miaka 6 na jinsi alivyopata majeraha hayo kutoka kwa mama mzazi hata hivyo  hali yake inaendelea vizuri.